Get New DJ Mixes
MUSIC

Mwendesha mazingaumbwe apotea mtoni wakati akijaribu kufanya miujiza hii nchini India

Mwendesha mazingaumbwe apotea mtoni wakati akijaribu kufanya miujiza hii nchini India
Mcheza kiini macho nchini India aliyejaribu kuiga muujiza maarufu kwa kuruka mtoni akiwa amefungwa mikono na miguu, na kutumbukizwa kichwa chini maguu juu, anahofiwa amefariki.nbChanchal Lahiri alijaribu kuiga kiini macho cha Harry Houdini – mcheza kiinimacho maarufu duniani – na alitarajiwa kujitatua na kutoroka, lakini hakuzuka kutoka kwenye mto huo uliopo katika jimbo la Bengal magharibi.
Watu waliokusanyika kushuhudia kiini macho hicho wamewaarifu maafisa wa polisi , ambao wameeleza kwamba wanamtafuta sasa. Lahiri, anafahamika kwa umaarufu kama Mandrake, alitumbukizwa ndani ya mto kutoka kwenye boti.
Alifungwa kwa makufuli sita na silisili au cheni wakati watu wakimtazama kutoka kwenye maboti mawili. Wengine wengi walikusanyika ufukweni katika daraja la Howrah huko Kolkata.
Polisi na kikosi cha wapiga mbizi wamepiga doria katika eneo hilo lakini kufikia jana Jumapili jioni, walikuwa hawajafanikiwa kumpata jamaa huyo.
Afisa mmoja amelieleza gazeti la Hindustan Times kwamba mpaka mwili wa Lahiri utakapopatikana, ndipo atakapothibitishwa kuwa amefariki.
Mpiga picha wa gazeti moja katika eneo hilo, Jayant Shaw, alishuhudia mkasa huo. Ameiambia BBC kwamba alizungumza na Lahiri kabla aanze kiini macho hicho.
“Nilimuuliza kwanini una hatarisha maisha yako kwa kiini macho,” Shaw amesema. “Lahiri alitabasamu na kusema, ‘Nikifanikiwa, ni miujiza, nisipofanikiwa basi litakuwa janga.’”
Mcheza kiini macho huyo alimueleza Shaw kwamba alitaka kufanya muujiza huo ili “kufufua shauku kwa kiinimacho”.
Hii sio mara ya kwanza kwa Lahiri kujaribu muujiza hatari wa chini ya maji.
Alitumbukizwa ndani ya mto uo huo ndani ya sanduku la kigae au glasi zaidi ya miaka 20 iliyopita lakini alifanikiwa kutoweka salama.
Shaw aliwahi pia kushuhudia kiini macho hicho cha awali chake Lahiri.
“Sikudhani kwamba hatofanikiwa kutoka ndani ya maji mara hii,” amesema.
By Ally Juma.

Leave a Comment